MOI YATOA MAFUNZO IDARA YA MAGONJWA YA NDANI HOSPITALI YA RUFAA SHINYANGA

Posted on: June 27th, 2023

Na SRRH

TAASISI ya Mifupa Muhimbili (MOI) imeanza kutoa mafunzo kwa Madaktari na Wauguzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Shinyanga wa Idara ya Magonjwa ya ndani (Internal Medicine), ili kuwajengea uwezo zaidi wa kutoa huduma za Afya.

Mafunzo haya yaliyoanza rasmi Jumatatu ya Juni 26, 2023, yanawezeshwa na Dkt. Hamis Shaffih Hamis pamoja na Muuguzi Dorcas Gideon Magawa (wote kutoka MOI), ambayo yatadumu kwa muda wa wiki moja hadi Juni 30, 2023.

Akizungumza wakati wa mafunzo, Muuguzi Magawa amesema lengo mama la mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo Watumishi wa Afya katika kuboresha kazi na kutoa huduma bora kwa za Afya kwa wagonjwa.

“Lengo kuwa la kutoa mafunzo haya ni kuhakikisha tunawajengea uwezo Madaktari ili waweze kuimarika vema katika utoaji wa huduma bora za Afya.

“Mafunzo haya yamelenga zaidi katika kutoa huduma za dharura kwa wagonjwa, hivyo tumekuja kutoa elimu zaidi ya nadharia na vitendo ili kuhakikisha huduma bora zinapatikana katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Shinyanga”, amesema Magawa.

Aidha, Magawa amewaomba Madaktari waliopata mafunzo hayo kuwa ni vema mafunzo haya yakaendelezwe kwa kuwasaidia Wataalamu wengine wa Afya kwa kuwafundisha ili kuhakikisha kunakuwa na wigo mpana wa huduma za Afya utakaosaidia kuongeza wingi wa wataalamu.

Katika kuboresha huduma za Afya na kuongeza uwezo kwa wataalamu, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Shinyanga imeendelea na utaratibu wake wa kawaida wa kuhakikisha inawejengea uwezo zaidi Madaktari wake kwa kuitisha mafunzo haya ili kukuza wigo na kutoa huduam bora za Afya kwa wananchi.